BIASHARA SIO MTAJI

Jeremiah Paul Wandili
8 min readJan 16, 2020

Ukisubiri upate Mtaji wa rasilimali fedha, ndipo uanze kufanya Biashara basi unaweza kuchelewa sana au kutofanya Biashara kabisa.

Biashara nyingi sio mpya, nyingi ni mwendelezo wa biashara zilizoanzishwa (kwa lugha nyepesi za urithi). Kwa sababu asili yetu ilikuwa katika mfumo wa ujamaa, hivyo maswala mengi yalifuata mfumo wa kushirikiana na kugawana sawa sawa.

Hivyo swala la biashara liliendeshwa kiujamaa (Mali ya Umma). Biashara nyingi zimeanza kufanyika mwishoni mwa miaka ya 80’s kiasi ambacho ilikuwa ngumu sana kuanza maana Sanaa ya biashara ilikuwa ni somo jipya sana.

Kwa kuwa historia ndio mwalimu mzuri utajikuta katika sehemu kubwa kati ya Familia 10, ni 3 tu ndio zilikuwa zinajishugulisha na biashara kwa ukubwa na wengine waliangukia kuwa walanguzi katika sekta ya kilimo na wachuuzi wa bidhaa katika biashara za watu wenye Asili ya Asia. Hivyo kwa tuliowengi dhana ya ujasiriamali na kufanya biashara bado ni masomo yanayoonekana kuwa magumu sana.

Kama msukumo wako wa kuanzisha biashara ni MTAJI, basi itakuchukua muda mrefu sana kuanza. Maana kila utakaposema fedha hizi zinatosha kuanza kisha unaingiwa na hofu na unajikuta unatumia fedha zote au sehemu ya fedha hizo katika shughuli nyingine.

Ndio maana kuna msemo usemao “Mwanzo wa kuanza ni kuanza” ikimaanisha ukitaka kuanza biashara anza na katika kuanza ndipo utaweza kuona changamoto na fursa katika kuanza.

Hivi karibuni kumetokea na hamasa kubwa sana katika kufanya biashara kama njia moja wapo ya kujiongezea kipato. Hii ni kutokana na upungufu mkubwa wa ajira na changamoto katika kupata kazi zinazoweza kukidhi mahitaji ya taaluma na maisha kwa ujumla.

Lakini pia wahamasishaji jamii wamewekeza nguvu kubwa kuwaeleza watu njia ya kutokea ikiwa ni kufanya biashara na kujishughulisha katika Ujasiriamali.

Na hivyo watu wengi wamekuwa na nia ya dhati kuyatafuta Maarifa ya biashara na Ujasiriamali. Na ndio maana wameibuka madalali wanaojifanya kuchanganua mawazo mbalimbali ya biashara.

Wameyafanya kuwa yananavutia sana na kuwashawishi watu kuwekeza katika Kilimo, Biashara za Masoko ya mtandao, ulanguzi na uchuuzi wa mtandaoni.

Kwa kuwa wengi wanatafuta kufanya vitu rahisi wengi wameishia kuumia na kulia kwa kupoteza fedha zao.

Kwa takribani miaka 5 sasa nimekuwa katika eneo la ushauri elekezi katika kuanzisha, kukuza na kuendeleza Biashara (Business Development Consultant). Nimekuwa nikipokea maswali na maombi mengi katika namna ya kuanzisha biashara. Maswali mengi sana ambayo kwa ujumla wake yamepelekea niandike Makala hii, iwe msaada kwa wote wenye maswali yanayofanana na haya;

· Nina kiasi cha fedha Shs. XXXXX ninaweza fanya biashara gani?

· Ninahitajika kuwa na kiasi gani cha fedha ndio nianze biashara?

· Biashara gani inalipa?

· Nina wazo hili la biashara ila sina Mtaji?

Kutokana na maswali ya namna hii, ambayo pasi na shaka yanathibitisha kuwa nia ipo na dhamira ni safi katika kutafuta mlango wa kutokea.

Kwa kuwa watu wengi wanajiita wahamaishaji wa fursa na biashara hawana hiyana, wao maswali haya kwao wamekuwa wanamajibu nayo kwa kila mtu na kila wakati.

Na hii imepelekea watu wengi kujikuta wanawekeza fedha zao au muda wao pasipo kupata matokeo tarajiwa na uishia kujilaumu.

Kwa kuwa Makala hii inalenga katika kujibu swali moja tu, la Nina fedha kiasi XXXXX nifanye biashara gani? Hivyo ntajikita kuelezea kwa kina mambo kadhaa yanayopeleka mtu kuanzisha na kuikuza biashara yake.

Kwanza kabisa ubunifu ndio nguzo muhimu sana katika kufikia wazo bora la biashara. Mawazo ya Biashara ni matokeo ya mawazo bunifu. Ndio, ubunifu ni nguzo muhimu sana katika kuchagua mawazo au wazo la biashara. Kwa namna gani unabadilisha changamoto kuwa fursa ya kibiashara na namna gani unaweza kuongeza thamani katika huduma au bidhaa ambayo imekuwa ikionekana ya kawaida.

Kwa kuwa watu wengi hawataki au kwa sababu zilizonje ya uwezo wao wanakosa kuwa wabunifu au ubunifu wanajikuta wanafanya yale yale au wanarudia mawazo ya biashara wanazoziona zikifanyika. Ndio maana kwa muda mrefu kumekuwa na mjadala usiofika mwisho wa watu kulalamika kuigana. Unakuta mtaa mmoja kuna biashara za namna moja ambazo hakuna anyejaribu kubadilika au kuweka ubunifu wa namna anavyo likabili soko.

Katika makala hii utajifunza dondoo kadhaa zitakazo kusaidia kuanzisha Biashara;

  1. Fahamu taarifa sahihi juu ya mahitaji ya wateja wako.

Kama wengi wasemavyo, kuwa bila utafiti hakuna haki ya kuongea (Kuchangia mjadala), vivyo hivyo katika biashara. Ili uweze kupata wazo la biashara, au unalo tayari wazo la biashara, ni muhimu kuandaa utafiti kwa kadri ya ukubwa wa biashara yako.

Msisitizo hapa ni utafiti unaoandaliwa wa kuonana na wateja tarajiwa, jamii kwa ujumla ili kujua nini wanahitaji au wangependa kupata huduma au bidhaa za aina gani. Usikubali kufanya utafiti kwa nijia ya mtandao, unaweza usikupe uhalisia stahiki, jitahidi kutenga muda na kuwatembelea wateja au wana jamii ili kuzungumza nao na kubadilisha nao taarifa.

Kwa kufanya utafiti utajifunza mambo mengi ambayo yataboresha ubunifu wako, wazo lako na mpango wako wa kufanya biashara. Usikubali kuhisi tu kuwa wateja watapenda vile unavyofikiria. Biashara nyingi zimeanzishwa na kufanyika kwa mapenzi ya waanzishaji na sio mahitaji ya wateja au jamii. Hivyo zinapoingia sokoni zinajikuta hazitoi matokeo tarajiwa.

Kwa makusudi kabisa, wengi wanajikuta kulaumu hali ya uchumi na kujion wasio na bahati. Nasisitiza wekeza katika kupata taarifa sahihi za kijeografia, hali ya wateja utakaowahudumia, uelewa juu ya bidhaa au huduma utakayoitoa.

2. Tafiti juu ya hali ya Soko na mifumo ya masoko.

Baada ya kuwa umeshakusanya taarifa sahihi za mahitaji ya wateja. Ni muhimu kufuatilia taarifa juu ya Soko, hapa utaangalia Zaidi, ukubwa wa soko, mahitaji ya wakati sokoni, muda wa kufanya biashara na kuangalia pia uwezo na nguvu za kulipia gharama katika bidhaa au huduma.

Kwa nyakati hizi za utandawazi, kumejitokeza fursa kubwa katika soko, la fursa hii ni soko la mtandao. Kabla haujaingia katika kulitumia soko la mtandao, uhisha taarifa kuhusu hali ya wateja ili kujua uelewa wao katika matumizi ya mtandao, Imani yao kuhusu biashara zinazofanyika mtandaoni.

Maana bila kujua mfumo bora wa soko, itakugharimu sana. Kuna watu waliposhauriwa katika kulitumia soko la mtandao, hawakufanya tafiti za kutosha wakafikia uamuzi wa kufunga sehemu zao za biashara ili kupunguza gharama za uendeshaji. Ikiwa ni pamoja na kulipia eneo la ofisi na kujikuta wanawekeza nguvu katika mtandaoni n kupata watazamaji wengi ila wakaishia kukosa wanunuzi.

Mifumo ya masoko ni pamoja na njia ya usambazaji, malipo na utayari wa kufungua masoko mapya na magumu kuingilika. Yote hiyo ni muhimu kufanya utafiti. Kwa kufanya utafiti pekee inakuongezea nguvu katika ubunifu na kutumia faida za hali ya soko kuongeza uwekezaji na kupunguza gharama za awali.

Hapa pia unaweza kutumia faida ya tafiti kuanza biashara pasipo mtaji mkubwa ua pasipo kabisa mtaji wa fedha. Ndio maana nilitamani kichwa cha Makala hii kiitwe, Biashara sio Mtaji, nikimaanisha sio mtaji wa rasilimali fedha tu kama wengi wanvyodhania.

3. Anzisha biashara kidogo kupima utayari na uhitaji wa Soko.

Katika mazungumzo yangu na wajasiriamali na wafanya biashara vijana nimejifunza kitu kikubwa sana. Kuna vijana wengi ambao wameanza kufanya biashara kwa kutumia ofisi za watu wengine. Kwa mfano, kijana mmoja yeye sio fundi “Ushonaji nguo” ila yeye amejigeuza mteja kwa baadhi ya mafundi, anachokifanya analekeza oda kwa fundi, kisha anapeleka picha mtandaoni (Instagram, Facebook na Whatsup) kisha anahamasisha wateja na kuzungumza nao biashara.

Kazi yake inabakia kuweza kumshawishi fundi katika gharama za ushanaji na kumshawishi mteja katika gharama za nguo. (Na bidhaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na Samani za Nyumbani, ofisini na katika nyumba za Ibada).

Biashara inavutia ikiwa kubwa, sasa basi epuka mtego huu. Kamwe usianzishe biashara kubwa wakati wa mwanzo. Wekeza kwa ukubwa katika kuijua biashara na anza kidogo kidogo. Katika kuanza utajifunza mambo mengi makubwa kwa vitendo.

Utajifunza mahitaji ya soko, utapokea oda za kusambaza bidhaa na kwa kadri ya muda utajikuta umesha panua wigo wa biashara na kujikuta unahudumia soko kubwa.

Ukianzisha kwa ukubwa unaweza kata tamaa katika hatua za awali ambapo ndio kwanza unajenga Imani kwa wateja na jamii. Unafahamu mahitaji yao kwa ujumla wake na kwa kuwa mauzo yatakuwa kidogo unaweza jikuta unakata tamaa na kuamua kufunga biashara.

4. Jenga mtandao na mfumo wa biashara yako.

Wakati unaanzisha biashara yako, kama ni ya kuuza bidhaa au kutoa huduma lazima pia ujue aina ya mfumo wa biashara yako kuanzia katika usimamizi na hata katika utawala na namna ya utoaji wa huduma.

Mtandao wa biashra yako ndio utakusaidia pia kujua aina ya wateja unao wahudumia na namna wao watakusaidia katika kukuza biashara yako. Je utanzisha mwenyewe au utakuwa na washika dau wengine ambao nao wataingia katika ngazi ya maamuzi.

Yapo mambo mengi ya kuzingatia aina ya mfumo wa biashara ila nitalijadili siku za usoni. Ila kwa sasa zingatia umuhimu wa kuwa na mtandao wa biashara yako hasa unajengwa na wateja. Kama ni kwa kutoa ofa au kwa kutoa mfumo wa kamisheni au kwa kutoa punguzo kwa kila mteja mpya anayeletwa.

Hii yote itapelekea kuwafanya wateja kumiliki biashara na kujiona ni sehemu ya mafanikio ya biashara kama utaweza mfumo mzuri na kujenga mtandao sahihi wa wateja.

Usiende Kariakoo/Wteja wakitafuta bidhaa na huduma katika Soko la Kariakoo

5. Wekeza Mtaji wa Fedha ili kuimarisha mfumo na mtandao wa biashara.

Wewe ni mmoja wa watu wanaofahamu kuwa Toa fedha upate fedha na kwa namna hiyo unaamini kabisa kuwa kuna nguvu katika rasilimali fedha katika kuanzisha biashara. Hivyo mimi pia siwezi kabisa kuikataa Imani hiyo.

Leo ninakupatia nafasi ya kuiweka fedha katika hatua ya mwisho. Wengi ambao walijihangaisha kuwekeza rasilimali fedha katika biashara zao kama kipaumbele cha kwanza, walijikuta wamefunga biashara zao au hata wao wenyewe kuingia katika migogoro (Kushindwa kulipa Madeni) na wadau wao katika biashara.

Msisitizo wangu hapa ni kuwa lazima ujue utaleta badiliko gani katika biashara na uzoefu huo ndio utakao amua ukubwa wa biashara unayoijenga na aina ya mtandao na mfumo wa biashara yako. Pasi na shaka utakuwa umenielewa kuwa ni kwa namna gani utazingatia mambo ya msingi yaliyotangulia. Huku ukijipanga kuwekeza rasilimali fedha.

Kwa kuhitimisha, nikwambie tu, hakuna wazo zuri au wazo baya. Mawazo yote ya biashara ni muhimu na ni mazuri inategemea na muktadha wa biashara itakapo fanyika.

Zaidi zingatia tu, kujua kuwa Maarifa na taarifa sahihi za biashara ndio nyenzo muhimu au ndio msingi wa mtaji wa biashara yako. Mjue na kumlinda Mteja. Mteja ni Mfalme wa Biashara.

Tumekuandalia mfululizo wa Makala za Anzisha Biashara Yako, Buni Wazo La Biashara na Mimi ni Masoko. Endelea kufuatilia na kuwashirikisha wengine. Zaidi tumeanzisha kundi la Whatsup kujiunga bofya hapa kujiunga Au wasiliana nami kwa +255655147271 Karibu, kwa ushauri elekezi katika Kukuza na Kuendeleza Biashara.

--

--

Jeremiah Paul Wandili

| Community Development | BDSPM Consultant| YALI Alumni, Founder & Executive Director @woteinitiative Youth Leadership Advisory Board, Member #YLAB @DOTTanzania